Tabora Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo alisema hakuna sababu kwa wanafunzi wanaosoma shule za vipaji maalum kupata alama ya ziro au daraja la nne kwenye mitihani yao ya mwisho badala yake wanafunzi hao wanapaswa kusoma kwa bidii ili waendane na sifa halisi ya shule hizo. Akizungumza jana mara baada ya kuzitembelea shule za wanafunzi wenye vipaji maalum za wavulana na wasichana za Tabora zilijukanazo kama ‘Tabora Boys’ na ‘Tabora Girls’ Waziri Jafo alisema kutokana na wanafunzi hao kuchaguliwa kwenye shule za vipaji maalum wanapaswa kusoma kwa bidii ili wafaulu kwa alama za daraja la kwanza na la pili na siyo vinginevyo.
Alisema kuwa hakuna sababu kwa wanafunzi wanaosoma shule za vipaji maalum nchini kuendelea kubaki kwenye shule hizo endapo viwango vya wanafunzi hao kwenye matokeo yao ya mitihani ya majaribio yataonyesha kuwa na ufaulu wa kawaida. “Kuanzia sasa nawaagiza wakuu wa shule za vipaji maalum kuwapeleka katika shule za kawaida wanafunzi wote walio katika shule za vipaji maalum ambao matokeo ya mitihani yao ya majaribio itaonyesha kuwa na ufaulu wa chini,” alifafanua Waziri Jafo na kuongeza: “Hatuhitaji mwanafunzi wa shule ya vipaji maalum apate division (daraja) III na kuendelea, endapo kwenye mtihani wake wa majaribio wa kidato cha pili atapata ufaulu hafifu, ina maana mwanafunzi huyo hastahili kuendelea kukaa kwenye shule hiyo.” Kwa mantiki hiyo Waziri Jafo alieleza kuwa kuanzia sasa kwenye shule zote za vipaji maalum watabakizwa wanafunzi waliofaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza na la pili kwenye mitihani yao ya kidato cha pili na wanafunzi watakaofaulu kuanzia daraja la tatu na kuendelea watapelekwa kwenye shule za sekondari za kawaida.
Kadhalika kwa wanafunzi wa kidato cha tano wanaochaguliwa kujiunga na shule za vipaji maalum wanapaswa kudhihirisha vipaji vyao kwa kuonyesha ufaulu wa daraja la kwanza kwenye mitihani yao ya kidato cha sita kama ilivyokuwa katika miaka ya 90 kurudi nyuma. Akiwa katika shule ya wavulana Tabora, Mhe.Jafo alionyesha masikitiko yake kutokana na kiwango cha ufaulu wa wanafunzi wa shule hiyo kuwa chini kiasi cha kuzidiwa na shule ya wasichana Tabora. Aliwataka walimu na wanafunzi wa shule hiyo kuongeza bidii ili shule hiyo iipite shule ya wasichana Tabora na endapo shule hiyo itafanya vizuri kwenye mitihani ijayo ya kidato cha sita, Mhe Jafo ameahidi kuwa mgeni rasmi kwenye mahafali yajayo ya wanafunzi wa kidato cha nne yatakayofanyika mwezi wa kumi mwaka huu.
Kwa upande wa shule ya wasichana Tabora nayo amewataka kuongeza bidii kwenye ufaulu wa mitihani ya kidato cha sita na kuwaahidi kugharamia chakula na pia kuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya kidato cha nne na pia kuwaalika wanafunzi wote wa kidato cha sita na wazazi wao endapo matokeo yajayo ya kidato cha sita, shule hiyo itafanikiwa kuwemo katika sita bora kitaifa. Mbali na kuzungumza na walimu na wanafunzi, Mhe.Jafo alipata fursa ya kujionea miundombinu iliyoboreshwa katika shule hizo ambapo kwa upande wa shule ya wavulana Tabora zaidi ya shilingi milioni 900 zilitumika kwenye ukarabati wa majengo ya shule hiyo ikiwemo ujenzi wa jengo la kisasa la maktaba ya shule hiyo.
Hata hivyo Mhe.Jafo alieleza kutoridhishwa kwake na kiasi kikubwa cha fedha kilichotumika kwenye ujenzi wa maktaba hiyo ambapo alisema kutokana na kiasi kilichotengwa kuwa kikubwa kilipaswa kutumika kwenye maktaba na miundombinu mingine Aidha Mhe.Jafo baada ya kutembelea miundombinu ya shule hiyo na kujionea ukarabati mkubwa uliofanyika alimwagiza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI kuhakikisha kuwa kuanzia sasa fedha zote zitakazopelekwa kwa ajili ya ukarabati wa shule kongwe 25 zilizochaguliwa ahakikishe kuwa shule hizo zinatumia mfumo wa 'force account' ili thamani ya fedha iendane na ukarabati wa majengo.
Naye Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia Elimu Bwana Tixon Nzunda aliwataka walimu na wanafunzi wa shule hizo kusoma kwa bidii kwani serikali ya awamu ya tano imetoa kipaumbele kwenye sekta ya elimu. Aliongeza kuanzia sasa anatarajia maafisa elimu wa wilaya na mikoa watazingatia kuwapendekeza walimu walioonyesha bidii kufaulisha kwa kiwango cha juu ili waweze kupandishwa vyeo. Wakati huo huo Bwana Nzunda alisema kuwa zaidi ya wanafunzi 100 waliokuwa wakisoma katika shule za vipaji maalum wakiwemo wanafunzi 11 kutoka shule ya wasichana Tabora wamepelekwa kwenye shule za kawaida baada ya kutofanya vizuri kwenye mitihani yao ya kidato cha pili. Shule za wavulana na wasichana za Tabora ni miongoni mwa shule zinazochukua wanafunzi wenye vipaji maalum kama zilivyo shule nyingine za aina hiyo za Mzumbe, Kibaha, Ilboru, Kilakala, na Msalato ya Dodoma
No comments:
Post a Comment